Je Ninapaswa Kula Machungwa Mangapi kwa siku? Chungwa Lina Faida gani Mwilini?


Chungwa ni tunda la mchungwa. Ni kati ya matunda yanayovunwa sana duniani. Jina la kisayansi ni Citrus aurantium L. var. sinensis L. au Citrus sinensis (L.) Osbeck. Ni jamii ya matunda aina ya citrus. Jamii hii ya matunda inajumuisha machungwa, machenza, tangarine, klementine  n.k.
Tunda lenyewe ni kijani na rangi inabadilika kuelekea njano ikiiva. Pamoja na limau, danzi, balungi na ndimu ni mojawapo kati ya matunda chungwa. na yanapatikana kwa wingi na urahisi sehemu mbalimbali hapa nchini. Machungwa ni matunda maarufu sana sehemu mbalimbali duniani ikiwemo Tanzania.

Asili yake ni katika Asia ya Kusini-Mashariki ambako lilioteshwa na wakulima. Kuna aina mbili yanayotofautiana kwa ladha ama chungu au tamu.
Aina yenye ladha chungu iliwahi kusambaa duniani hivyo jina la Kiswahili limetunza ladha hii hata kama matunda mengi yanayopandwa siku hizi ni aina tamu.
Chungwa tamu lilisambaa kote duniani baada ya Wareno kuchukua machipuko yake na kuyapanda kwanza Ureno baadaye hata Amerika na Afrika kuanzia karne ya 15.


Figure 1: Chungwa Tunda na Juisi/Sharubati Yake

Virutubisho Vinavyoaptikana Katika Machungwa.
Machungwa yana mkusanyiko wa virutubisho vingi; Wanga, Protini kwa kiasi kidogo, Vitamini (A, B1,B2,B3,B5,B6,B9, C, E) madini (Kalsiam,Chuma, Zinki,Potasiam) na kambakamba (roughage/fibers).
Machungwa ni chanzo kikubwa na kizuri cha Vitamini C katika mlo. Chungwa la ukubwa wa wastani lina miligramu 50 za Vitamini C, na kwa kawaida mahitaji kwa siku ya Vitamini C ni miligramu 90 kwa mwanaume na miligramu 75 kwa mwanamke. Hivyo chungwa moja au mawili kwa siku yanaweza kutosheleza mahitaji hayo.
Machungwa yanaweza kuliwa kama tunda zima au kwa kunywa juisi ya machungwa. Juisi ya machungwa huwa na virutubisho vyote vya machungwa isipokuwa kambakamba (roughage/fibers), ambazo zipo kwa wingi zaidi  mtu napokula chungwa zima.

Figure 2: Machungwa yaliyovunwa tayari kwa matumizi mbalimbali

Kiwango cha asidi
Kama ilivyo kwa jamii ya matunda ya citrus, machungwa nayo huwa na hali ya aside, yenye kiwango cha pH karibu na 2.5 -3, kulingana na umri wake, ukubwa na aina ya chungwa. Japo si kama ilivyo kwa limao, bado machungwa huwa na kiwango cha asidi cha kutosha
Figure 3: Chati ya viwango vya PH


Je Ninapaswa Kula Machungwa Mangapi kwa siku?
Inashauriwa kula chungwa moja au mawili kwa siku, kwani hii hutosheleza mahitaji ya Vitamin C na madini mengine mwilini. Ulaji wa machungwa mengi sana(zaidi ya 50) kwa siku unaweza kusababisha kujaa Vitamini C (hypervitaminosis) ambako ni hatari kwa afya.
Kumbuka kuwa hata chungwa moja tu ukila lina kidhi yale mahitaji muhimu ya mwili ya kila siku (daily requirement), iwe chungwa lenyewe au juisi yake halisi.

Figure 4: Chungwa Lililoiva Vyema


Faida za Machungwa:
  • Huimarisha Kinga ya Mwili.
Vitamini C pamoja na madini mengine ikiwemo Zinki, yanatumika kwenye ufanyaji kazi wa mfumo wa kinga ya mwili.
  • Hupunguza Hatari ya Magonjwa ya Moyo na Saratani.
Machungwa yana kampaundi ziitwazo phytochemicals kama hesperedin, ambazo hulinda mishipa ya damu na kupunguza lehemu (cholesterol) kwenye damu.Vitamini C pia iliyopo kwenye machungwa huondoa sumu za mwili (free radicals), ambazo huchangia kutokea kwa saratani na magonjwa ya moyo zinapokuwa zimelundikana mwilini.
  • Huimarisha afya ya fizi na mdomo.
Vitamini C husaidia kujenga protini za kolajeni za fizi za mdomoni, hii huimarisha afya ya fizi. Ukosefu wa Vitamini C mara nyingi huambatana na fizi kuvuja damu kutokana na kukosa protini za kolajeni za kutosha.
  • Hupunguza lehemu(cholesterol) mwilini.
Machungwa yana kambakamba laini (soluble fibers) ambazo huyeyuka kwenye chakula. Hizi husaidia kunyonya mafuta ya lehemu(cholesterol) yaliyo kwenye chakula na kutolewa nje ya mwili kama choo. Hii hupunguza mafuta ya lehemu(cholesterol) kwenye mwili wa mtu.
  • Kuona vizuri.
Machungwa yana Vitamini A ambayao inasaidia kuhakikisha macho yanaona vizuri, pamoja na kamapundi nyingine ambazo hulinda tishu za macho zisiharibiwe na mwanga.
  • Hupunguza hatari ya kukosa choo/kupata choo kigumu (constipation).
Machungwa hasa pale mtu anapokula chungwa zima, humpatia kambakamba ambazo husaidia kulainisha chakula kwenye utumbo na kukifanya choo kuwa laini.
  • Huimarisha afya ya ngozi.
Madini yaliyopo kwenye machungwa pamoja na Vitamini A na C husaidia kujenga na kuondoa seli za ngozi zilizokufa.

Fanya machungwa kuwa sehemu ya mlo wako kila siku ufaidike na kazi zake.
😇😇😇

0 comments:

Post a Comment